Friday, October 19, 2012

HOTUBA YA MENEJA MPANGO WA TAIFA WA KUDHIBITI UKIMWI KATIKA MKUTANO WA KURASIMISHA MATOKEO YA UTAFITI ULIOFANYA MIONGONI MWA WANAWAKE WANAOFANYA BIASHARA YA NGONO DAR ES SALAAM UKUMBI WA Dar es Salaam International Conference Centre – DAR ES SALAAM, 19 OCTOBER, 2012

Kaimu Mganga Mkuu  Wa Serikali, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Donnan Mmbando

Mwenyekiti, tume ya Taifa ya kudhibiti UKIMWI
Mganga Mkuu wa Mkoa Dar es Salaam
Mratibu wa UKIMWI wa Mkoa wa Dar es Salaam na Manispaa
Wawakilishi wa taasisi za kitaifa na kimataifa
Wawakilishi wa watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI
Ndugu wana habari
Wageni Waalikwa
Mabibi na Mabwana:

Kwanza kabisa, kwa niaba ya Mpango wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI, ninapenda kutoa shukrani za dhati kwa nyote mliojumuika hapa katika tukio hili muhimu la kuwasilisha  ripoti ya utafiti uliofanywa miongoni mwa wanawake wanaofanya biashara ya ngono hapa Dar es Salaam. Vilevile, ninapenda kuchukua fursa hii kuwakaribisha washiriki wote katika mkutano huu mliokubali kujumuika nasi katika tukio hili muhimu katika kuongeza kasi ya mapambano dhidi ya UKIMWI nchini.

Ndugu Washiriki,
Shukurani maalum nazielekeza kwa Kaimu Mganga Mkuu  -  Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Donnan Mmbando kwa kukubali na kulibeba jukumu la kuwa mgeni rasmi katika mkutano huu. Kuhudhuria kwako ni faraja kubwa kwetu.  Tunakushukuru wewe binafsi ukiwa kama Kaimu Mganga Mkuu kwa kufuatilia kwa karibu  matukio ya UKIMWI nchini na kuhakikisha mapambano dhidi ya UKIMWI yanaendelezwa.

Ndugu Washiriki,
Katika maandalizi ya kuandaa mikakati ya kupambana na UKIMWI miongoni mwa makundi yaliyo katika hatari zaidi ya kupata maambukizi ya VVU, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ikishirikiana na CDC ilifanya utafiti miongoni mwa wanawake wanaofanya biashara ya ngono  ili kufahamu hali ya maambukizi ya VVU. Tunatambua kuwa kila mmoja wetu yuko katika hatari ya kuambukizwa VVU ila kuna makundi ambayo yako katika hatari zaidi kutokana na tabia na mienendo yao.  Mpango wa Taifa wa kudhibiti UKIMWI ulifanya utafiti miongoni mwa wanawake wanaofanya biashara ya ngono hapa Dar es Salaam mnamo mwaka 2009-2010. Zoezi hilo ambalo lilifanyika mwishoni mwa mwaka 2009 lilijumuisha mkoa wa Dar es Salaam na linategemewa pia kufanyika mikoa mingine hasa yenye maambukizi makubwa ya VVU. Wakati wa zoezi hilo, wadau wanaojihusisha na mapambano dhidi ya UKIMWI katika ngazi ya taifa, mkoa, wilaya na jamii walishiriki katika kutoa taarifa mbalimbali zinazohusu makundi haya. Vilevile wadau waliweza kubainisha mafanikio, changamoto na mahitaji ya makundi yaliyo katika hatari zaidi ya kupata maambukizi ya VVU  miongoni mwa walengwa mbalimbali.

Ndugu Washiriki,
Kwa kutumia matokeo hayo, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeweza kubaini changamoto mbalimbali na hali ya maambukizi miongoni mwa wanawake wanaofanya biashara ya ngono na kubaini mbinu mbalimbali za kuweza kuwafikia na  kukabiliana na tatizo hili. Wizara pia imeweza kubaini mahitaji ya kimawasiliano, elimu, tiba kinga na huduma ya taarifa sahihi juu ya UKIMWI miongoni mwa walengwa katika afua za Virusi vya UKIMWI na UKIMWI. Binafsi ninaamini kwamba, sisi tuliokusanyika hapa leo tutakuwa wajumbe wazuri katika kujadili ripoti hii na kuweza kuona ni jisi gani tunaweza kuyafikia makundi haya. Kwa mara nyingine, natoa shukrani za dhati kwa mikoa, wilaya na wadau wote walioshiriki katika zoezi la ukusanyaji wa takwimu zilizosaidia kupata ripoti hii.

Ndugu Washiriki,
Kwa ridhaa yenu, nachukua fursa hii kumkaribisha mkurugenzi wa DCD Tanzania kuzungumza na ninyi machache na baada ya hapo mgeni rasmi ili kwanza azungumze na washiriki wa mkutano na hatimaye afungue rasmi mkutano huu muhimu wa uzinduzi wa ripoti ya kwanza iliyotoa picha ya tatizo la maambukizi ya UKIMWI miongoni mwa wanawake wanaofanya biashara ya ngono na jamii kwa ujumla.

Karibu Mgeni Rasmi



No comments:

Post a Comment