Friday, October 19, 2012

HOTUBA YA MGENI RASMI KATIKA MKUTANO WA KUWASILISHA RIPOTI YA UTAFITI ULIOFANYIKA DAR ES SALAAM MIONGONI MWA WANAWAKE WANAOFANYA BIASHARA YA NGONO– UKUMBI WA DAR ES SALAAM INTERNATIONA CENTER – DAR ES SALAAM, 19 OCTOBA 2012



Mkurugenzi  Msaidizi  wa Afya na Usafi wa Mazingira na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Kinga Elias Chinamo wakati alipokuwa akiongea na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Mratibu wa UKIMWI wa Mkoa Dar es Salaam
Waratibu wa UKIMWI wa Wilaya za Dar es Salaam
Wawakilishi wa taasisi za Kitaifa na Kimataifa
Wawakilishi wa taasisi za dini
Wawakilishi wa mitandao wa watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI
Wawakilishi wa taasisi zinazofanya kazi na makundi yaliyokatika hatari zaidi ya kuambukizwa UKIMWI.
Ndugu waandishi wa habari
Wageni Waalikwa
Mabibi na Mabwana:

Awali ya yote, ninapenda kuwafahamisha kwamba ninayo furaha kubwa ya kujumuika nanyi leo kwenye tukio hili muhimu katika mustakabali wa mapambano dhidi ya janga la UKIMWI nchini Tanzania. Kama mlivyotaarifiwa kwamba, mkutano huu wa siku moja ni mahsusi kwa ajili ya usambazaji wa ripoti ya utafiti uliofanyika Dar es Salaam mwaka 2010 miongoni mwa wanawake wanaofanya biashara ya ngono.

Ndugu Wageni Waalikwa,
Niwashukuru ninyi nyote mliopata nafasi ya kuhudhuria mkutano huu muhimu. Nawashukuru kwa sababu naamini kwamba nyote mnaunga mkono  juhudi za serikali katika  mapambano dhidi ya janga la UKIMWI, na kwamba baada ya mkutano huu wengi wenu kama si wote mtashiriki katika kuandaa mikakati ya kuweza kupunguza maambikizi ya UKIMWI miongoni mwa makundi haya na hata mtakaporudi katika sehemu zenu za kazi, ninaamini mtakuwa mabalozi wazuri wa utekelezaji huo.

Ndugu Washiriki,
Sote tunafahamu kwamba mlipuko wa UKIMWI  kwa muda mrefu umeathiri maisha ya Watanzania wengi, pamoja na uchumi na maendeleo ya nchi yetu.  Kila familia imeathirika kwa namna moja au nyingine.  Kadhalika,  sote tumekuwa tukijitahidi kupambana na mlipuko huu kwa njia nyingi tofauti tukishiriakiana na vyombo vya habari, asasi za kiraia, taasisi za dini zote, wahisani wa maendeleo na wanajamii kwa ujumla.  Tunakiri kuwa mabadiliko yapo – japokuwa sio kwa kiwango na kwa haraka ambayo tungependa iwe.  Wapo walioweza (na hasa vijana) kusubiri wasijiingize katika mambo ya kujamiiana mapema kabla ya wakati unaofaa baada ya ndoa.  Wapo ambao wamekuwa waaminifu katika ndoa zao.  Wapo pia walioshindwa katika hayo mawili lakini wameweza kutumia kondomu ili kujikinga dhidi ya maambukizi. Na wapo pia walioshindwa kutumia njia mojawapo ya hizo kutokana na shughuli wanazofanya au mazingira wanapoishi.

Ndugu Washiriki wa mkutano,
Katika kipindi cha takriban miongo mitatu ya kuwepo kwa janga la UKIMWI nchini, Serikali na wadau mbalimbali katika mapambano dhidi ya UKIMWI wamekuwa wakifanya juhudi za makusudi ili kuhakikisha adui UKIMWI anatokomezwa hapa nchini. Juhudi hizi, zimekuwa zingilenga aidha kuzuia maambukizi ya Virusi vya UKIMWI au kutoa huduma ya tiba na matibabu kwa watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI. Hata hivyo, suala la makundi hatarishi limekuwa ni suala mtambuka miongoni mwa afua zote zinazolenga mapambano dhidi ya UKIMWI.

Ndugu Washiriki,
Ikumbukwe kwamba, hivi sasa kuna taasisi na asasi mbalimbali za kitaifa na kimataifa zinazojishughulisha na utoaji wa huduma za afya, mbinu za kujizuia na kupambana na tatizo la UKIMWI miongoni mwa makundi haya. Kwa kutumia mbinu mbalimbali, taasisi hizi zimechangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa ufahamu kuhusu janga la UKIMWI hapa nchini. Lakini pia, kuwepo kwa taasisi na asasi hizi kunapelekea watanzania kupata taarifa kutoka katika vyanzo mbalimbali. Hata hivyo, juhudi hizi bado kwa kiasi kikubwa zimejikita kwa mikoa michache na bado hazijaweza kufikia makundi yote. Wakati huo huo, wizara ilikuwa inakosa takwimu sahihi za kujua maambukizi na kuweza kutengeneza mikakati ya kitaifa kupambana na janga la UKIMWI miongoni mwa makundi hatarishi.

Ndugu Washiriki wa Mkutano,
Kwa kuzingatia kwamba, hakuna takwimu halisi za kujua hali ya maambukizi miongoni mwa makundi yaliyo katika hatari zaidi ya maambukizi ya UKIMWI, Wizara ya Afya kupitia Mpango wa Taifa wa kudhibiti UKIMWI kwa msaada wa CDC ikishirikiana na vyuo vikuu vya Muhimbili na Mlimani walifanya utafiti mwaka 2009-2010 ili kujua hali ya maambukizi miongoni mwa wanawake wanaofanya biashara ya ngono. Lengo la utafiti lilikua ni pamoja na kuweza kujua hali ya maambukizi ili kuweza kutengeneza mikakati sahihi ya kutokomeza UKIMWI miongoni mwa makundi haya na jamii nzima kwa ujumla.Vilevile, ripoti hii itatoa mwangaza wa kuweza kutengeneza mikakati mbalimbali ya kumbana na UKIMWI na makundi mengine yaliyo katika hatari ya kupata maambukizi ya UKIMWI pia.

Ndugu Washiriki,
Michango mingi ya wadau katika mapambano dhidi ya janga la UKIMWI nchini, imekuwa ikitolewa huku kukiwa na ushirikiano mdogo miongoni mwa wadau wenyewe katika sekta ya umma na sekta binafsi. Hii imepelekea matumizi mabaya ya rasilimali kwa kudurufu kazi zinazofanywa na wadau mbalimbali ili kufikia malengo yaliyokusudiwa. Baadhi ya sababu zinazosababisha ufanisi usioridhisha wa kuyafikia makundi yote na kuweza pia kwa kiwango kikubwa:
  • Ushirikishwaji hafifu  wa mikakati ya kuyafikia makundi haya kwa upande wa serikali na  na taasisi zinazotoa huduma husika.
  • Kushindwa kuyafikia makundi yaliyo katika hatari zaidi ya kupata maambukizi aidha kwa kuwa sheria za nchi haziruhusu baadhi ya tabia wanazozifanya hivyo kusababisha kazi zao kufanyika kificho.

Ndugu Wageni Waalikwa,
Wazo la kufanya utafiti huu katika sekta ya afya linatoka katika Mpango Mkakati wa Pili wa Mapambano dhidi ya UKIMWI katika sekta ya afya wa mwaka 2008/2012. Kwa kuwa hakukua na takwimu sahihi za kuonyesha hali ya maambukizi miongoni mwa makundi haya hapa nchini, baadhi ya taasisi zimekuwa zikitoa huduma ya kupambana na UKIMWI kwenye makundi haya bila ya kuwa na takwimu halisi za hali ya maambukizi. Kwa kulitambua hilo, Wizara ya Afya  na Ustawi wa Jamii kupitia Mpango wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI imeamua kutoa takwimu hizi ili kuweza kutoa mwongozo kwa wahisani, mikoa na wilaya kuhusukutengeneza mikakati ya kupambana na UKIMWI kwa makundi yaliyo katika hatari zaidi ya kupata maambukizi ya UKIMWI Taarifa hizi zitasaidia makundi haya kuweza kupata huduma za Virusi vya UKIMWI na UKIMWI zinazotolewa na Wizara ya Afya kama vile huduma ya Ushauri Nasaha na Upimaji wa Virusi vya UKIMWI na huduma za dawa za kupunguza makali ya Virusi vya UKIMWI na magonjwa ya ngono na via vya uzazi. 

Wageni Waalikwa,
Mafanikio ya kupatikana kwa repoti hii yameweza  kupatikana kutokana na  juhudi na rasilimali mbalimbali zilizotolewa na Serikali na wadau wake. Tunawashukuru sana  wadau wetu kwa kuelewa nia yetu na kutuunga mkono katika juhudi za mapambano dhidi ya janga la UKIMWI nchini.

Kwa namna ya pekee napenda kuwataja wadau wa maendeleo  wafuatao ambao wamechangia katika kufanikisha upatikanaji wa repoti hii: 
·         Serikali ya Marekani kupitia Shirika lake la misaada ya  kituo cha Kudhibiti Magonjwa Tanzania (CDC)
·         Chuo kikuu cha tiba Muhimbili
·         Chuo kikuu cha Dare s salaam sehemu ya mlimani
·         Shirika la AMREF
·         Maabara ya kitaifa ya NIMR Tanzania
Tunawasihi wenzetu wote hawa na wengine waendelee kutuunga mkono katika mapambano dhidi ya janga la UKIMWI hapa nchini hadi azma yetu ya ‘Tanzania bila UKIMWI’ itimie.

Wageni Waalikwa,
Katika mapambano ya aina yoyote ile ni lazima umfahamu adui yako vizuri, ufahamu yuko wapi na ana silaha gani.  Kwa kufahamu hivyo utaweza kujiandaa vilivyo kuweza kukabiliana naye.  Adui yetu hapa ni UKIMWI na siyo mtu anayeishi na virusi vya UKIMWI. Ili kuweza kukabiliana naye, kila mmoja katika nafasi yake hana budi kushika silaha na kupambana na adui huyu hatari kwa mustakabali wa taifa letu. Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa upande wake inaendelea kubuni mbinu mbalimbali zinazohitajika ili kusimamia na kuendeleza mapambano ya UKIMWI kwa ufanisi mkubwa. Mapambano yakienda vizuri, kama tunavyokusudia, naamini ipo siku sote tutafurahia matunda yake.

Wageni Waalikwa,
Waandishi wa habari mnafanya  kazi nzuri sana katika juhudi za kupambana na UKIMWI hapa nchini.  Kupitia kwenu, jamii imeweza kupata taarifa na kuongeza uelewa kuhusu Virusi vya UKIMWI na UKIMWI. Napenda kutoa shukurani za dhati kwenu na kuwasihi muendeleze mapambano hayo. Lakini pia ninawasihi kutoa taarifa sahihi zilizofanyiwa uchunguzi wa kina kuhusu  janga la UKIMWI. Aidha, viongozi wa dini nanyi pia tunatambua na kuthamini mchango wenu katika mapambano dhidi ya janga la UKIMWI hapa nchini. Ninafarijika sana na kampeni zinazoongozwa hususan na viongozi wa madhehebu ya Kikristo na Kiislam kuhusu kuepuka maambukizi ya Virusi vya UKIMWI.  Nanyi pia nawasihi muendeleze mapambano haya ili sote kwa pamoja tushinde mapambano haya.

Wageni Waalikwa,
Napenda kumalizia hotuba yangu kwa kuwasihi nyote muwe mabalozi wazuri katika utumiaji wa taarifa hizi ili kuweza kutengeneza mikakati sahihi ya kupambana na UKIMWI miongoni mwa makundi yaliyo katika hatari zaidi na jamii nzima kwa ujumla.Lengo letu liwe kuongeza chachu ya mapambano dhidi ya UKIMWI hapa nchini.

No comments:

Post a Comment